Pages

Friday, March 13, 2015

POLISI KUCHUNGUZA KUHUSIANA NA MADAI YA DOKTA WILBROAD SLAA


Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limeanza kuchunguza malalamiko ya Katibu Mkuu wa Chadema Dk Wilbroad Slaa ya kutaka kulishwa sumu na Mlinzi wake.

Madai hayo ambayo yamekuwa gumzo katika vyombo vya habari wiki hii huku wananchi wakihoji uhalisia wake, yamemuhusisha mlinzi huyo wa Dk Slaa huku yeye mwenyewe akikataa tuhuma hizo na kudai kuwa ameteswa na walinzi wa chadema.

Kamanda wa kanda maalum ya Dar es Salaam Suleiman Kova  amesema hayo  leo alipokuwa akizungumza  na waandishi wa habari ofisini kwake kuhusu taarifa hizo zilizofikishwa katika kituo cha polisi cha Oysterbey kupitia wakili wa Chadema John Malya ambae aliambatana  na  mtuhumiwa Khalid Kagenzi (48) ambaye ni mlinzi wa Dk. Slaa ili akatoe maelezo kwa niaba yake.

Mlinzi wa Dk. Slaa alidai kuwa ana majeraha mwilini yaliyotokana na mateso aliyofanyiwa akiwa chini ya ulinzi mkali  wa maafisa wa usalama wa Chadema ambao walikaa naye na kumhoji kuanzia tarehe 07/03 saa tano asubuhi hadi tarehe 08/03 mwaka huu saa kumi jioni.

Aidha Kamanda Kova amesema kuna mambo mawili yanafanyiwa uchunguzi likiwemo la mlinzi Khalid Kagenzi  na la pili ni dhidi ya watuhumiwa wanaodaiwa kumtesa kwa kumshambulia  mlinzi huyo  na kumsababishia majeraha mwilini mwake.

Kova aliwataja watuhumiwa wanaoshikiliwa na Jeshi la Polisi kwa kosa la shambulio la kudhuru mwili ni  Boniface Jacob, (32) mkazi wa kisiwani Ubungo, ambae ni diwani kata ya Ubungo kupitia Chadema,Hemed Ally Sabula (48) mkazi wa Tandale kwa Tumbo ambae Afisa Usalama wa Chadema,Benson Mramba (30)mkazi wa Tabata Kisukuru ,Afisa Utawala wa Chadema.

Aliongeza kuwa watuhumiwa hao watatu wapo chini ya ulinzi kwa makosa yaliyotajwa dhidi ya Khalid Kagenzi  na shauri litafikishwa mahakamani  kupitia kwa wakili wa serikali ili kujiridhisha  kisheria  na hatimaye kutoa maamuzi kuhusu mashtaka yao.

No comments:

Post a Comment