Pages

Friday, March 13, 2015

JKT WAAGIZWA KUWAJENGEA NYUMBA WAATHIRIKA WA MVUA YA MAWE KAHAMA

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ameliagiza Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kuwajengea nyumba 403 mpya waathirika ambao walibomolewa nyumba zao kutokana na mvua kubwa, yenye mawe na upepo mkali iliyonyesha usiku wa Machi 3, 2015, katika vijiji vitatu vya Kata ya Mwakata, Wilaya ya Kahama, Mkoa wa Shinyanga.
Aidha, Rais Kikwete amesema kuwa Serikali itaendelea kuwatunza na kuwapatia huduma zote za msingi watu walioathiriwa na maafa ya mvua hiyo hadi watakapokuwa na uwezo wa kujitegemea wenyewe.
Rais Kikwete pia amesema kuwa maafa ya mvua hiyo yasitumike kama kisingizio cha watu kulipiza kisasi kwa madai kuwa mvua hiyo ilinyesha kutokana na msukumo wa kishirikina.
Rais Kikwete ameyasema hayo, leo, Machi 12, 2015,wakati alipohutubia mkutano mkubwa wa hadhara wa wananchi katika Kata ya Mwakata, Wilaya ya Kahama, Mkoa wa Shinyanga, ambako anafanya ziara maalum ya siku mbili kutoa pole kwa wananchi wa vijiji vitatu vya kata hiyo walioathirika na mvua iliyonyesha usiku wa Machi 3, 2015.
Rais Kikwete amewaambia wananchi hao: “Nimekuja kuwapeni pole kutokana na maafa ya mvua. Napenda kuwahakikishieni kuwa Serikali iko nanyi. Msiba wenu ni msiba wetu, huzuni yenu ni huzuni yetu na machungu yenu ni machungu yetu.”
Rais Kikwete amewaambia wananchi kuwa Serikali itaendelea kuzikarabati nyumba ambazo ziko katika hali ya kukarabatiwa. “Zile za ukarabati tutaendelea kuzikarabati na zile zilizoharibika kabisa tutazijenga. Naambiwa zinahitaji kiasi cha Sh. Bilioni mbili, tutazitafuta na tutajenga kwa vyovyote vile. Naambiwa kuwa ni nyumba 403 mpya. Hakuna atayepewa fedha taslim, na wala mtu asije kuomba fedha, ili ajenge mwenyewe. Na wala zamu hii hakuna tenda kwa sababu tutatumia Jeshi letu la kujenga taifa – tayari nimewaambia waifanye hii kazi. Hii ni dharura na chombo chetu cha dharura ni Jeshi letu.”
Rais Kikwete pia amewashukuru wote ambao wamekuwa wanatoa misaada ya kusaidia wahanga wa mvua hiyo, ikiwa ni pamoja na wale ambao wametoa makazi ya dharura kwa waathirika na misaada mingine.
Rais Kikwete pia amesema kuwa Serikali itaendelea kutoa misaada ya dharura kwa waathirika hadi watakapokuwa na uwezo wa kujitegemea wenyewe: “Tayari Serikali imetoa tani 20 za chakula, tumetoa mafuta na sukari. Tutaendelea kuwaunga mkono mpaka mvuke. Aidha, hakuna yoyote ambaye atapoteza maisha kwa sababu ya ukosefu wa chakula. Tayari kuna chakula cha kutosha mwezi mmoja mpaka mwezi ujao na kikiisha tutaleta kingine.”
Rais Kikwete ameongeza: “Tutakabiliana pia na magonjwa ya mlipuko. Tayari tuna kituo cha dharura cha afya na kinatoa huduma mzuri.”
Rais Kikwete ameamuru uongozi wa Mkoa wa Shinyanga kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Kahama kuhakikisha kuwa yananunuliwa magodoro ya haraka ili watoto waweze kulala vizuri na kuepukana na magonjwa ya vichomi.
“Magodoro yatapatikana kesho, yapo hapa Kahama na kama hakuna yafuatwe hata Shinyanga. Lakini lazima yapatikane kesho (Ijumaa, Machi 13, 2015). Naambiwa mahitaji ya magodoro ni 649, tayari 558 yamepatikana na bado yapo mahitaji ya magodoro 149 na haya tutaleta kesho,”amesema Rais Kikwete.
Kuhusu imani za ushirikina ambazo zinaanza kuandamana na tukio la mvua hiyo, Rais Kikwete amesema: “Msijiingize katika mambo ya ushirikina na ramli. Mvua za mawe ni za kawaida duniani hata kama hazijapata kunyesha hapa. Msitoke hapa kwenda kutafuta waganga kuhusiana na mvua hii ili mpate sababu ya kuua watu.”
Ameongeza: “Mvua za namna hii ni matukio ya kawaida na maisha ya kawaida katika maeneo mengine. Hakuna mchawi hapa, bali ni rehema za Mwenyezi Mungu. Nimesikia sikia mambo haya. Hayana kichwa wala miguu. Hili ni tukio la kawaida.”
Amesisitiza Rais Kikwete: “Napenda kuwahakikishia kuwa Serikali yenu ipo. Acheni kuamanika, acheni kubabaika. Asiwababaishe mtu yoyote. Leo nimekuja mwenyewe mkubwa wa Serikali. Watakuja wengi kuwadanyanga, hawana Serikali. Wakija waambieni hivi – mwenye Serikali tuliyemchangua kaja, keshatuahidi, chakula tunakula, huduma za awali tumezipata na hizo nyingine amesema atatutimizia. Ili kuja kuwapeni pole mwambieni awapeni pole tu, asiwababaishe.”
Imetolewa na;
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu – Dar es Salaam.
12 Machi, 2015

No comments:

Post a Comment