
Utangulizi
Ndugu Wananchi;
Kama
ilivyo ada tunamshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutuwezesha
kuzungumza kupitia utaratibu wetu huu mzuri wa hotuba za kila mwisho wa
mwezi. Kwa mwisho wa mwezi wa Februari nina mambo matano ninayopenda
kuyazungumzia.
Zoezi la Uandikishaji Wapiga Kura
Ndugu Wananchi;
Jambo
la kwanza ni uandikishaji wa Wapiga Kura. Tarehe 24 Februari, 2015
Waziri Mkuu, Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda alizindua rasmi
uandikishaji wa wapiga kura ikiwa ni sehemu ya zoezi la uboreshaji wa
daftari la kudumu la wapiga kura nchini. Zoezi hili lilizinduliwa
Makambako, Mkoani Njombe na litaendelea nchini kote mpaka
litakapokamilika kwa mujibu wa ratiba itakayopangwa na Tume ya Uchaguzi.
Uandikishaji unatumia teknolojia ya kisasa ya utambuzi wa alama za
vidole (BVR) na macho ya mtu anayeandikishwa. Teknolojia hii itatusaidia
kuondoa kutoaminiana, manung’uniko na madai kuhusu udanganyifu katika
chaguzi zetu kwamba wamepiga kura wasiostahili. Kuanza kutumika kwa
teknolojia hii ni kielelezo cha utashi wa Serikali kuwa nchi yetu iwe na
chaguzi zilizo huru, wazi na haki.
Ndugu Wananchi;
Mtakumbuka
kuwa, kabla ya uzinduzi wa zoezi hili, Tume ya Taifa ya Uchaguzi
ilifanya zoezi la majaribio ya uandikishaji wa wapiga kura kwa kutumia
mashine za teknolojia hii mpya katika kata 10 katika Halmashauri za
Kinondoni, Kilombero na Mlele kati ya tarehe 15 hadi 23 Desemba, 2014.
Habari
njema ni kuwa, kwa kutumia mashine za BVR, idadi ya waliojiandikisha
ilivuka lengo la uandikishaji kwa kipindi kilichopangwa katika Kata
hizo. Katika Halmashauri ya Kilombero walioandikishwa walifikia asilimia
110.9 ya lengo, katika Halmashauri ya Mlele uandikishaji ulifikia
asilimia 101 ya lengo na katika Jimbo la Kawe, katika Halmashauri ya
Wilaya ya Kinondoni walioandikishwa walikuwa asilimia 105.67 ya lengo.
Mafanikio haya ni ya kutia moyo pamoja na changamoto za kiufundi
zilizojitokeza na zile zinazotokana na upya wa mfumo wenyewe kwa
watumiaji. Changamoto hizo zimefanyiwa kazi na watengenezaji wa vifaa
vinavyotumika katika awamu hii ya uandikishaji wa wapiga kura nchi
nzima.
Ndugu Wananchi;
Nimefarijika
na taarifa kuwa zoezi la uboreshaji wa Daftari na uandikishaji wa
wapiga kura limeanza vizuri Makambako. Wananchi wamejitokeza kwa wingi
kuliko ilivyotarajiwa. Kati ya tarehe 23 hadi 25 Februari, 2015 kwa
mfano, Tume ilitegemea kuandikisha wapiga kura 9,541 lakini kutokana na
mwamko wa wananchi kuwa mkubwa wameweza kuandikisha wapiga kura 13,042.
Kila kituo kilikuwa kinaandikisha kati ya wapiga kura 80 na 150 kwa
siku. Lengo la Tume ni kuandikisha wapiga kura 32,000 katika Halmashauri
ya Makambako ambako kwa siku wanatarajia kuandikisha watu 4,320.
Naambiwa kuwa hesabu za juzi na jana wameandikisha hadi wapiga kura
6,000 kwa siku. Kwa kasi hii na kama mambo yatakwenda kama
inavyotarajiwa, lengo hilo litafikiwa na hata kuvukwa.
Ndugu Wananchi;
Hatuna
budi kutoa pongeza kwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa hatua hii ya kutia
moyo tuliyofikia katika mchakato huu. Inaondoa hofu iliyoanza kuingia
miongoni mwa baadhi ya watu kuwa huenda zoezi hili lisingefanikiwa.
Tunachokitaka kwa Tume ni kuona zoezi hili linaendelea na kukamilika
kama ilivyopangwa. Napenda kurudia ahadi niliyokwishaitoa kwa Tume
kwamba Serikali itafanya kila linalowezekana kuiwezesha kirasilimali ili
iweze kutimiza jukumu lake hilo. Nimekwishawakumbusha Hazina kuhusu
umuhimu wa zoezi hili kufanikiwa kama ilivyopangwa. Hivyo basi,
nimewataka wahakikishe kutoa kipaumbele cha kwanza katika mgao wa fedha.
Kama haifanyiki nawaomba Tume waniambie mimi mwenyewe.
Wito
wangu kwenu, wananchi wenzangu, ni kujitokeza bila ya kukosa kwenda
kujiandikisha kwa mujibu wa ratiba ya uandikishaji katika maeneo yenu
kama itakavyotolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi. Msifanye ajizi maana
hakutakuwepo na fursa nyingine ya kujiandikisha kabla ya Uchaguzi Mkuu
wa mwaka huu baada ya fursa hii kupita.
Ndugu Wananchi;
Kama
ilivyoelezwa na Tume na mimi kusisitiza mara kadhaa kuwa
watakaojiandikisha wakati huu ndio watakaopiga kura ya maoni kuhusu
Katiba Inayopendekezwa na ndio watakaopiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa
Oktoba, mwaka huu. Vitambulisho vya zamani vya mpiga kura havitatumika,
hivyo watu wote ambao ni Watanzania na wana umri wa miaka 18 au zaidi
lazima wajitokeze kuandikishwa upya. Watu pekee ambao hawatapaswa
kujiandikisha tena ni wale tu walioandikishwa katika zoezi la majaribio
lililofanyika katika zile kata 10 za Halmashauri za Kinondoni, Ifakara
na Mlele mwezi Desemba, 2014. Vitambulisho walivyopata ndivyo vyenyewe.
Ndugu Wananchi;
Napenda
kutumia nafasi hii pia kuwaomba viongozi wa vyama vya siasa, Serikali,
dini na asasi za kiraia kuungana na Serikali na Tume ya Uchaguzi katika
kuwakumbusha na kuwahamasisha wananchi wakajiandikishe. Naomba
tusiwachanganye wananchi kwa kutoa taarifa zisizokuwa za kweli na
kuwafanya wakaacha kujiandikisha. Sisi katika Serikali tunafanya kila
linalowezekana kuhakikisha kuwa kila atakayejitokeza kujiandikisha
anaandikishwa. Aidha, tutahakikisha kuwa kila panapojitokeza changamoto
zinatafutiwa ufumbuzi kwa wakati mwafaka.
Tunatambua
kuwa mfumo huu ni mpya hivyo panaweza kujitokeza changamoto
zinazosababishwa na upya wake. Nawaomba wahusika kuendelea kuwaelimisha
watendaji wanaohusika ili wapate uzoefu unaostahili. Aidha, nawasihi
wananchi kuwa wavumilivu na waelewa pale ambapo wakati mwingine
watalazimika kukaa kwenye mistari kwa muda mrefu kusubiri kujiandikisha,
au wakalazimika kuja siku ya pili.
Ndugu Wananchi;
Kupiga
kura kuamua kuhusu Katiba Inayopendekezwa au kuchagua Rais, Wabunge na
Madiwani ni haki na wajibu wa kila raia. Lakini, kuipata haki hiyo na
kuweza kutimiza wajibu huo kunategemea kuwa na kitambulisho cha mpiga
kura. Bila ya hivyo haiwezekani. Haya shime jitokezeni, mjiandikishe,
ili muweze kuitumia haki yenu na kutimiza wajibu wenu wa kuipigia kura
Katiba Inayopendekezwa na kuchagua viongozi mnaowaona wanafaa kuongoza
nchi yetu, jimbo lako na kata yako.
Kura ya Maoni
Ndugu Wananchi;
Jambo
la pili ninalotaka kulizungumzia ni kuhusu Kura ya Maoni ya Katiba
Inayopendekezwa. Kama mjuavyo, baada ya Bunge Maalumu la Katiba kutunga
Katiba Inayopendekezwa na Rais kuchapisha Katiba hiyo katika Gazeti la
Serikali na kutangaza siku ya kupiga kura ya maoni, kinachoendelea sasa
ni matayarisho ya kufanyika kwa kura hiyo. Yapo majukumu ya Serikali,
yapo majukumu ya Tume ya Uchaguzi, na yapo majukumu ya Serikali na Tume
kwa pamoja. Utekelezaji umeishaanza na unaendelea. Miongoni mwa mambo
yanayotakiwa kufanyika ni uandikishaji wa wapiga kura ambao
umekwishaanza na unaendelea.
Ipo
pia kazi ya kuchapisha na kusambaza Katiba Inayopendekezwa ili wananchi
waweze kuisoma na kuielewa kabla ya kupiga kura ya maoni. Tayari Katiba
Inayopendekezwa imetangazwa katika tovuti za Wizara ya Katiba na
Sheria, Wizara ya Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo na katika tovuti
ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Pia imechapichwa magazetini.
Hadi
tarehe 27 Februari, 2015 vitabu 1,558,805 vilikuwa vimechapishwa na
nakala 1,341,300 kusambazwa. Nakala 1,141,300 zimesambazwa kwenye mikoa
25 ya Tanzania Bara na nakala 200,000 zimegawiwa kwa Zanzibar. Kwa
upande wa Tanzania Bara kila Kata imepewa vitabu 300. Kwa vile Kata zina
wastani wa vijiji vitano (5) hii ina maana kwamba kila kijiji kimepata
vitabu 60 kwa kila kijiji ambayo si haba.
Ndugu Wananchi;
Tume
ya Uchaguzi itatoa maelekezo kuhusu utaratibu wa kutoa elimu kwa umma.
Nimeambiwa tayari asasi za kiraia 420 kwa upande wa Bara na 75 kwa
upande wa Zanzibar zimejiandikisha kwa ajili ya zoezi hilo.
Halikadhalika, Tume itatoa maelekezo husika kuhusu kampeni ya Kura ya
Maoni wakati ukiwadia. Naomba watu wawe na subira na kuzingatia masharti
ya Sheria ya Kura ya Maoni na Kanuni zake. Tukifanya hivyo, zoezi hili
muhimu na la kihistoria litatekelezwa kwa usalama na utulivu. Watu
watafanya uamuzi kwa uhuru, uelewa, amani na usalama.
Hali ya Usalama Nchini
Ndugu wananchi;
Jambo
la tatu ninalotaka kulizungumzia ni hali ya usalama nchini. Kwa jumla
hali ya usalama ni nzuri, hata hivyo kuna matukio ya kiusalama ambayo
ningependa kuyazungumzia. La kwanza ni mashambulizi yenye sifa za
ujambazi na mwelekeo wa kigaidi. Na, la pili ni la mauaji ya watu wenye
ulemavu wa ngozi.
Katika
kipindi cha miezi 12 hivi kumekuwa na matukio ya watu kuvamia vituo vya
Polisi, wengine wanachoma moto au wengine wanapora silaha. Pia
kumekuwepo na matukio ya kuwashambulia Polisi walioko kwenye doria na
wengine kuporwa silaha. Vituo vya Polisi vilivyovamiwa na silaha kuporwa
ni vya Newala Mkoani Mtwara silaha tatu ziliporwa, Ikwiriri katika
Wilaya ya Rufiji silaha saba, Kimanzichana, Wilaya ya Mkuranga silaha
tano, mbili za polisi na tatu za raia waliokwenda kuzihifadhi pale, na
Ushirombo Wilaya ya Bukombe silaha 18. Pugu Machinjioni na Tanga, askari
waliokuwa katika shughuli za ulinzi na doria walishambuliwa na kuporwa
silaha tatu. Kule Songea kulikuwepo na matukio mawili ya Polisi
kushambuliwa lakini silaha hazikuporwa.
Bahati
mbaya, vijana wetu saba wa Jeshi la Polisi walipoteza maisha katika
matukio hayo. Newala alikufa Polisi mmoja, Kimanzichana mmoja, Ikwiriri
wawili, na Ushirombo watatu. Wapo Polisi kadhaa waliopata majeraha ya
namna mbalimbali katika mashambulizi haya.
Ndugu Wananchi;
Silaha
zote 18 zilizoporwa Ushirombo zimepatikana na watu 10 wanaotuhumiwa
kuhusika na uhalifu huo wamekamatwa. Katika tukio la Tanga silaha moja
kati ya mbili zilizoporwa imepatikana. Watuhumiwa saba wametiwa mbaroni,
wanne kati yao ni wale waliokuwa wamejifisha katika mapango ya Kiomoni
katika Kitongoji cha Karasha-mikocheni, kilichoko kijiji cha Mzizima
wilayani Tanga. Tayari watu wanne wanaotuhumiwa kuhusika na tukio la
Ikwiriri wamekamatwa. Polisi wanaendelea na upelelezi kuwapata watu
wengine na kuzipata silaha saba zilizoporwa kituoni hapo. Kwa tukio la
Newala silaha zote tatu zimepatikana pamoja na bastola moja ya mtuhumiwa
aliyehusikaa na watu wawili wametiwa nguvuni. Hali kadhalika, upelelezi
unaendelea wa kuzipata silaha zilizoporwa ambazo hazijapatikana mpaka
sasa: yaani Kimanzichana moja, Pugu Machinjioni moja na Tanga iliyosalia
moja.
Ndugu Wananchi;
Matukio
haya yana sura mbili. Yana sura ya ujambazi, lakini pia baadhi yake
yana dalili za ugaidi. Vyombo vyetu vya usalama vinaendelea kufanya kazi
yake ya uchambuzi wa kila tukio na kulipa nafasi yake stahiki. Napenda
kutumia nafasi hii kutoa pongezi za dhati kwa Jeshi la Polisi
wakishirikiana na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania na vyombo
vingine vya usalama kwa kazi kubwa na nzuri waifanyayo kupambana na
uhalifu nchini. Mafanikio tunayaona, kama nilivyoeleza na kama
tulivyosikia kule Tanga hivi karibuni ni matunda ya ushirikiano huo.
Hata hivyo, nimewataka waendelee kuwasaka watu hawa waovu po pote walipo
ili wafikishwe mahakamani na kuzirejesha mikononi mwa Polisi silaha
zote zilizoporwa.
Nawaomba
wananchi wenzangu wote kushirikiana kwa karibu na vyombo vya usalama
hususan Jeshi la Polisi ili tuweze kupata mafanikio zaidi dhidi ya
uhalifu huu na uhalifu mwingineo. Nawaomba mfanye mambo mawili: Kwanza,
toeni taarifa Polisi mnapozipata habari za vitendo viovu au nyendo za
watu waovu wanavyokusudia kufanya wahalifu au taarifa za wale
waliokwishafanya uhalifu.
Pili,
naomba watu waache kuwashabikia watu hawa waovu wala kueneza taarifa
zao potofu kwenye mitandao ya kijamii. Badala yake tutumie mitandao ya
kijamii kuponda fikra zao potofu, fikra zao hasi na vitendo vyao viovu
pamoja na kuwafichua wao na mambo yao mabaya wayafanyo. Napenda kutumia
nafasi hii kuwashukuru na kuwapongeza wananchi wote walioweza kutoa
taarifa zilizowezesha kuzuia uhalifu usifanyike au zilizowezesha kutiwa
mbaroni kwa wahutumiwa wa vitendo vya ujambazi na ugaidi. Hatuwezi
kushinda uhalifu bila ushirikiano baina ya wananchi na vyombo vya ulinzi
na usalama.
Mauaji ya Watu Wenye Ulemavu wa Ngozi
Ndugu wananchi;
Nimesikitishwa
sana na taarifa kuwa mauaji ya ndugu zetu wenye ulemavu wa ngozi
(Albino) yameibuka upya baada ya hali kuwa tulivu mwaka 2011. Mwaka jana
(2014) yalitokea matukio matatu katika mikoa ya Mwanza, Tabora na
Simiyu na mwaka huu limetokea tukio moja mkoani Geita.
Lazima
tulaani vikali mauaji ya ndugu zetu albino. Ni vitendo vya kinyama
ambavyo havitegemewi kufanywa au kutokea katika jamii yeyote ya watu
waliostaarabika, ya watu wanaomuabudu Mungu. Watu wenye ulemavu wa ngozi
ni wanadamu wenzetu, wenye haki sawa ya kuishi na kupata hifadhi ya
maisha yao kama walivyo wanadamu wengine. Hawastahili kufanyiwa
wanayofanyiwa. Hawapaswi kuishi kwa hofu katika kijiji chao, mtaa wao au
katika nchi yao. Jamii nzima na sisi sote mmoja mmoja na katika umoja
wetu, tunao wajibu wa kuhakikisha usalama wa maisha yao na mali zao kama
ilivyo kwa watu wengine wote.
Kwa
kweli, mauaji ya albino ni jambo linalofedhehesha na kulidhalilisha
taifa letu. Ni vitendo visivyovumilika. Hatuna budi sote kushikamana na
kuhakikisha kuwa tunapambana nao kisawasawa na kuwashinda. Tusikubali
kamwe wakaturudisha kule kubaya tulikokuwa zamani. Naungana na Chama cha
Albino Tanzania kulaani ukatili huu na kutaka watu wote wanaojihusisha
na ukatili huu wasakwe, wakamatwe, wafikishwe Mahakamani na kupewa
adhabu kali inayowastahili wanapopatikana na hatia.
Ndugu Wananchi;
Napenda
kuwahakikishia kuwa wakati wote Serikali imelipa uzito mkubwa suala la
kudhibiti na kukomesha mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi au kukatwa
baadhi ya viungo vyao wenyewe wakiwa hai. Tumefanya hivyo bila ya
kuchoka tangu tukio la kwanza baada ya mimi kuingia madarakani Aprili
17, 2006 na miezi mitatu tu kule Nyahunge, Geita alipouawa Alfa Amon
ambapo watuhumiwa wawili waliuawa na raia. Mwaka 2007 kulikuwa na
matukio saba. Mwaka 2008 ndio ulikuwa mwaka mbaya sana walipouawa watu
18.
Kutokana
na jitihada kubwa zilizofanywa na Serikali kwa kushirikiana na wananchi
mauaji yalipungua na kuwa tisa mwaka 2009. Mwaka 2010 kukawa na tukio
moja na mwaka 2011 hapakuwepo na tukio lolote. Mwaka 2012 kukawa na
tukio moja, mwaka 2013 aliuawa mtu mmoja na wawili kujeruhiwa. Mwaka
2014 waliuawa watu watatu na wawili kujeruhiwa, na Januari, 2015
kumetokea tukio moja kule Geita.
Ndugu Wananchi;
Tangu
mwaka 2006 mpaka 2015, watuhumiwa 139 wametiwa nguvuni, miongoni mwao
wako watuhumiwa 16 wa matukio ya Desemba na Januari mwaka huu. Mashauri
35 yamefunguliwa mahakamani na kati ya hayo 10 bado yanaendelea na yapo
katika hatua mbalimbali. Watuhumiwa 73 wameachiliwa na 15 wamepatikana
na hatia. Kati ya hao waliopatikana na hatia 13 wamehukumiwa kifo na
wawili wamepata kifungo cha miezi 6. Watuhumiwa kwa matukio sita bado
wanasakwa.
Matukio
ya mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi yametokea katika mikoa kumi
kati ya mikoa 30 hapa nchini. Mikoa hiyo ni hii ifuatayo: Mwanza matukio
13, Kagera sita, Tabora matano, Geita manne, Mara manne, Kigoma manne,
Simiyu matatu, Shinyanga mawili, Arusha moja na Mbeya moja. Utaona
matukio 41 kati ya 43 yametokea katika ukanda wa ziwa ambapo pia
wanaongoza kwa mauaji ya vikongwe na wanawake kwa sababu za ushirikina.
Ndugu Wananchi;
Inawezekana
kuwa matukio ya hivi karibuni yanaashiria kuwa uhalifu huu unataka
kuibuka upya. Napenda kuwahakikishia ndugu zetu wenye ulemavu wa ngozi
na Watanzania kwa jumla, kuwa hatutaacha hali iwe mbaya kama ilivyokuwa
miaka ya nyuma. Tutatumia mbinu na maarifa tuliyoyatumia kukabili wimbi
kubwa la mauaji lililokuwepo mwaka 2007 na 2008 na kwa sababu hiyo
tukaweza kupunguza hadi kufikia kutokuwa na tukio lolote la mauaji mwaka
2011.
Tunachokiomba
kutoka kwa wananchi ni ushirikiano na msaada wa kuwafichua watu
wanaofanya vitendo vya mauaji na kukata viungo vya watu wenye ulemavu wa
ngozi. Pia wasaidie kutoa taarifa kuhusu wanunuzi wa viungo hivyo na
waganga wanaochochea mahitaji ya viungo vya albino. Ushirikiano wa
wananchi wa wakati ule uliwezesha kupatikana kwa mafanikio niliyaeleza.
Naamini safari hii tukifanya hivyo tutafanikiwa pia.
Ndugu Wananchi;
Kutokomeza
kabisa matukio ya mauaji na ukataji wa viungo vya watu wenye ulemavu wa
ngozi ni jambo linalowezekana. Hata hivyo, litategemea watu kuacha
imani za ushirikina. Imani potofu, ati kuwa mtu akiwa na kiungo cha mtu
mwenye ulemavu wa ngozi atafanikiwa katika shughuli zake za biashara,
uvuvi na uchimbaji wa madini ndicho kichocheo cha uovu wote huu
unaoendelea. Ni ujinga ulioje kwa mtu kuamini kuwa mafanikio yake
hayatategemea juhudi zake na maarifa yake bali kuwa na kiungo cha
mwanadamu mwenzake mwenye ulemavu wa ngozi.
Nilisema
katika hotuba yangu ya mwisho wa mwezi Machi, 2008 kwamba, kama kuwa na
kiungo cha albino ndiko kutakakomfanya mtu kufanikiwa katika shughuli
zake za kibiashara na kiuchumi basi ndugu zetu wenye ulemavu wa ngozi
wangekuwa ndiyo matajiri wakubwa nchini na duniani. Maana wao sio tu
wana viungo bali wana mwili mzima. Kwa sababu ya kuwepo imani hizi za
hovyo, juhudi za kuelimisha jamii kuachana na imani hizi potofu
ziongezwe. Naomba hili ndilo liwe jambo la msingi katika mapambano haya.
Tukifanikiwa katika hili, matatizo yote haya yatakoma. Serikali na
jamii haitalazimika kushughulikia mambo haya ambayo siyo tu ni fedheha
hata kumsimulia mtu bali yanatisha na kusikitisha.
Ndugu Wananchi;
Wiki
ijayo nitakutana na baadhi ya viongozi na wanachama wa Chama cha Watu
Wenye Ulemavu wa Ngozi. Nimekubali maombi yao ya kukutana nao ili niweze
kusikiliza maoni yao na tubadilishane mawazo juu ya namna bora ya
kumaliza tatizo hili. Mimi naamini kuwa ushirikiano wa karibu kati ya
Serikali na jamii utatuwezesha kutokomeza mauaji ya ndugu zetu wenye
ulemavu wa ngozi na kuliondolea taifa letu aibu hii.
Ziara ya Zambia
Ndugu Wananchi;
Tarehe
25 na 26 Februari, 2015 nilifanya ziara ya siku mbili ya kiserikali
nchini Zambia kwa mwaliko wa Rais mpya wa nchi hiyo, Mheshimiwa Edgar
Lungu. Ziara ilikuwa na mafanikio makubwa. Mimi na ujumbe wangu
tulifarijika sana kuona kuwa mawazo ya nchi zetu mbili yanashabihiana
sana kuhusu namna ya kuimarisha na kuboresha uhusiano wetu na
ushirikiano na uhusiano wa nchi zetu mbili. Kimsingi tumekubaliana
katika masuala yote muhimu tuliyoyazungumza.
Kuhusu
TAZARA tumekubaliana kuchukua hatua thabiti kutatua matatizo ya
kiungozi, kifedha na kiufundi yanayolikabili shirika letu hilo hivi
sasa. Tumeelewana kuwa hatuna budi kufanya marekebisho ya kimfumo na
kiutendaji ili kutatua matatizo ya kimuundo na kimenejimenti
yanayochangia kuzorota kwa ufanisi wa Shirika. Tumekubaliana pia kuwa,
Serikali zetu mbili zitekeleze ipasavyo wajibu wake kwa TAZARA ikiwa ni
pamoja na kutoa mchango wake wa fedha kwa ajili ya kulifufua Shirika
hili muhimu kwa uchumi wa nchi zetu mbili.
Ndugu Wananchi;
Tumekubaliana
pia, kwamba, tuangalie uwezekano wa kuruhusu makampuni au mashirika
mengine ya reli kutumia reli ya TAZARA kusafirishia mizigo yao kwa
kulipa ushuru kwa TAZARA kwa huduma hiyo. Tumeagiza Baraza la Mawaziri
kulifanyia kazi wazo hili jema ili litekelezwe mapema iwezekanavyo.
Kwa
upande wa sekta ya nishati, tumekubaliana kuwa, nchi zetu mbili
ziendelee kushirikiana kuimarisha bomba la mafuta la TAZAMA. Ndugu zetu
wa Zambia walitueleza dhamira yao ya kutaka kujenga bomba la kusafirisha
gesi kutoka Dar es Salaam hadi Zambia. Wameomba tukubali kuwauzia gesi
asilia. Niliwaeleza ni jambo linaowezekana, tumekubaliana nchi zetu
zilifanyie kazi ombi hilo.
Serikali
ya Zambia, imeahidi kuimarisha njia ya umeme kutoka Kasama hadi Mbala
Zambia inakoanzia njia inayoleta umeme Sumbawanga. Kufanya hivyo
kutaondoa matatizo ya sasa ambapo umeme unaofika Sumbawanga kutoka Mbala
huwa mdogo kiasi kwamba hauna nguvu ya kutosha kwa matumizi ya
nyumbani, maofisini na viwandani. Kwa sababu hiyo, hata mpango wa
kuupeleka umeme huo Namanyere, Nkasi na Mpanda haukuweza kutekelezwa
kama ilivyokuwa imekusudiwa awali.
Ndugu Wananchi;
Kuhusu
kuboresha huduma kwa abiria na mizigo katika mpaka wa Tanzania na
Zambia pale Tunduma, tumekubaliana kuwa, Serikali ya Tanzania ikamilishe
ujenzi wa jengo litakalowezesha huduma zote muhimu za mpakani kutolewa
katika jengo hilo (One Stop Border Post). Wakati tunasubiri kukamilisha
ujenzi huo, tumekubaliana tuwe na jengo la muda la kurahisisha taratibu
za usafiri wa abiria na usafirishaji wa mizigo katika mpaka wetu na
Zambia.
Vilevile,
tulizungumzia njia za kuimarisha na kuboresha taratibu za forodha kwa
mizigo itokayo bandari ya Dar es Salaam kwenda Zambia na Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Kongo kupitia Zambia. Tumekubaliana kuwa, Mamlaka ya
Kodi ya Mapato ya Zambia iangalie uwezekano wa kuwaweka maafisa wake
katika Bandari ya Dar es Salaam kama inavyofanyika kwa nchi wanachama wa
Jumuiya ya Afrika Mashariki. Hii itarahisisha taratibu za forodha kwa
bidhaa za Zambia katika bandari yetu. Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo
imeshaanza mchakato wa kupata fursa hiyo. Kwa jumla, ziara ilikuwa ni
yenye mafanikio makubwa.
Rambirambi
Ndugu Wananchi;
Wakati
tulipokuwa tunajiandaa kurekodi hotuba hii tukapata habari ya huzuni na
majonzi makubwa ya kifo cha Mbunge wa Mbinga Magharibi, Mheshimiwa
Capt. John Damian Komba. Kifo chake kimeliondolea taifa letu mmoja wa
viongozi wake wazuri, msanii mahiri, raia mwema na mzalendo wa kweli.
Marehemu alitumia muda mwingi wa maisha yake kuelimisha jamii kuhusu
mambo mema, amefanya hivyo akiwa mwalimu na baadaye Kiongozi wa Kikundi
cha Sanaa cha JWTZ na hapa mwishoni kiongozi wa kikundi cha Tanzania One
Theatre cha Chama Cha Mapinduzi. Kwa kutumia kipaji alichojaaliwa na
Mola wake ametoa mchango mkubwa kwa maendeleo ya nchi yetu na ustawi wa
Chama Tawala. Daima tutamkumbuka kwa mambo mengi mema aliyoifanyia jamii
ya nchi yetu na taifa kwa jumla.
Ndugu Wananchi;
Katika
salamu zangu za rambirambi kwa Spika wa Bunge na Katibu Mkuu wa CCM
niliwaomba kupitia kwao salamu ziwafikie Wabunge wote na viongozi na
wanachama wa Chama Cha Mapinduzi. Hali kadhalika, niliomba kupitia kwao
salamu ziwafikie familia ya marehemu Capt. John Komba. Kwa familia ya
ndugu yetu mpendwa, napenda kuwahakikishia kuwa tuko pamoja nao katika
kipindi hiki kigumu cha majonzi na maombolezo. Tunawaombea kwa Mola
awape moyo wa subira na uvumilivu. Wananchi wa Wilaya ya Nyasa tunawapa
pole nyingi kwa msiba mkubwa uliowakuta na pengo kubwa mlilolipata.
Nawaomba watambue kuwa namna bora zaidi ya kumlilia Mbunge wao
aliyewapenda ni kudumisha mema yote aliyofanya na kukamilisha zile kazi
ambazo alikusudia kuzifanya lakini hakuweza kufanya hivyo kwa sababu ya
kukutwa na umauti.
Mwisho nawaomba, Watanzania wote tuungane na familia yake kumwombea marehemu Capt. John Damian Komba mapumziko mema. Amin.
Mungu Ibariki Afrika!
Mungu Ibari ki Tanzania!
Asanteni kwa kunisikiliza.